Mamlaka za usalama nchini zimefanikiwa kuwakamata watu kadhaa wanaodaiwa kuhusika na mtandao wa kughushi kadi za benki na kujipatia zaidi ya shilingi bilioni 147.5 kupitia njia za udanganyifu wa kifedha.
Tuhuma hizo, ziliibuliwa katika taarifa ya Mkurugenzi Mkuu wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) ya mwaka wa fedha 2024/25, Chrispin Chalamila aliyoiwasilisha mbele ya Rais Samia Suluhu Hassan Machi 30, 2026.
Kwa mujibu wa taarifa ya Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania (BoT), Emmanuel Tutuba, watuhumiwa hao wanaoaminika kuwa raia wa kigeni walikuwa wakitumia teknolojia ya kisasa kunakili taarifa za kadi halisi za wateja wa benki, kisha kuiba fedha kutoka kwa wateja bila ridhaa yao.
Aidha, uchunguzi umebaini fedha zilitolewa kupitia malipo ya huduma na bidhaa kwa kutumia kadi 1,551 za wateja wa mataifa 11 kupitia kampuni 162 na benki tano za Tanzania, na kwamba kadi hizo zilitumika kufanya malipo mbalimbali ya huduma za utalii, usafirishaji, malipo ya kodi na bima ya afya.